RC MTAMBI AKABIDHI MKOPO WA BIL. 1.02 KWA VIJANA BBT-UVUVI

Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Mtambi amekabidhi mitaji yenye thamani ya Shilingi Bil. 1.02 kwa vijana wanufaika wa Programu ya Jenga kesho iliyo bora upande wa sekta ya Uvuvi (BBT-UVUVI) kwenye hafla iliyofanyika Mei 28,2026 kwenye Ufukwe wa Tembo eneo la Lakeside mkoa Mara. Akizungumza mara baada ya kukabidhi mitaji hiyo iliyojumuisha jumla ya vizimba 40 kwa vijana 40 Kanali Mtambi amewataka vijana hao kuhakikisha wanasimamia vizuri mradi huo ili uweze kuwapa matokeo wanayotarajia. “Lakini la pili mhakikishe kuwa mnaposimamia vizuri mnafata zile kanuni na maelekezo ya ufugaji bora wa samaki na la tatu ni kuhakikisha wakati mnaendelea na mchakato wote huu kile mnachopata mnakirejesha ili kuwawezesha vijana wengi zaidi kupata mikopo hiyo” Ameongeza Mhe. Kanali Mtambi. Aidha Kanali Mtambi ameahidi kuwa mlezi wa wanufaika hao ambapo amewataka wataalam kuhakikisha wanawatembelea mara kwa mara na kuwapa ushauri wa kitaalam ili kuongeza tija kwenye ufugaji wao.