ASUBUHI YA TAHARUKI SOKO LA MANYEMA - MOSHI

Kulipokuwa kunaanza kuamka kwa shughuli za kawaida za biashara katika Soko la Manyema, Manispaa ya Moshi, wafanyabiashara walikuwa wamepanga nyanya, vitunguu, ndizi, nafaka na mboga mboga wakisubiri wateja wa kwanza wa siku. Lakini ndani ya sekunde chache, utulivu huo uligeuka kuwa taharuki. Mayowe ya watu yakaanza kusikika. "Lori... lori... kimbieni!" baadhi ya mashuhuda walikuwa wakipaza sauti huku kila mmoja akitafuta njia ya kuokoa maisha yake. Lori lenye namba T488 DMN, ambalo kwa mujibu wa mashuhuda lilikuwa limetokea eneo la Riadha, lilidaiwa kufeli breki na kuanza kushuka kwa kasi bila dereva kulidhibiti. Wafanyabiashara waliokuwa wameinama wakipanga bidhaa zao hawakuwa na muda wa kufikiria mara mbili. Wengine walikimbia huku wakiacha bidhaa zao, wengine walijaribu kuwaonya wenzao, huku wengine wakijikuta wamenaswa na vifusi vya vibanda vilivyoporomoshwa na lori hilo. Ndani ya muda mfupi, eneo lililokuwa limejaa sauti za biashara likageuka kuwa eneo la mayowe, vumbi na harakati za uokoaji. Nyanya zilitapakaa barabarani, magunia ya mahindi na mchele yakachanika, mizani ikaporomoka na mabati ya vibanda yakakunja kama karatasi mbele ya nguvu ya lori hilo. Mashuhuda wanasema lori hilo lilianza kuonyesha dalili za kufeli breki likiwa eneo la Riadha kabla ya kuingia kwa kasi katika mitaa ya Manyema na hatimaye kuvamia vibanda vya wafanyabiashara ndani ya soko.