Hatua Kubwa Ufugaji Zanzibar! Kikundi cha Bambi Chapewa Ardhi ya Malisho

Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo, Mhe. Suleiman Masoud Makame, ameagiza kutolewa hekari tano kwa kikundi cha Wafugaji wa Maendeleo Kwanza cha Bambi, kwa ajili ya kuimarisha uzalishaji wa chakula cha mifugo. Agizo hilo amelitoa akiwa katika muendelezo wa ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa Kusini, Wilaya ya Kati, alipokutana na wafugaji wa Bambi wanaonufaika na mradi shirikishi wa wasindikaji na wazalishaji wa maziwa Tanzania — Ti3P, ambapo tayari wamepatiwa ng’ombe 19. Aidha, Waziri Suleiman Masoud Makame ameielekeza Idara ya Maendeleo ya Mifugo kuchagua watu wawili kutoka katika kikundi hicho ambao watakwenda mkoani Arusha kujifunza mbinu bora za ufugaji kwa mfugaji aliyepiga hatua, ili kuongeza ujuzi na ushirikiano baina ya wafugaji. Kwa upande wake, Kiongozi wa Wafugaji wa Maendeleo Kwanza, Bwana Hamid Abdallah, ameishukuru Serikali kwa kuwapatia eneo la malisho na kwa kuwashirikisha wafugaji katika kila hatua ya utekelezaji. Ameahidi kuendeleza jitihada za kuongeza uzalishaji wa maziwa kupitia ng’ombe waliopatiwa. Mradi huu wa Ti3P umeendelea kuwanufaisha wafugaji Zanzibar, ambapo hadi sasa jumla ya ng’ombe 246 zimetolewa — ng’ombe 93 Unguja na ng’ombe 153 Pemba katika lengo la kuongeza upatikanaji wa maziwa kwa uhakika nchini.