MBOLEA ZA ORGANIC ZAPIGIWA CHAPUO

Kupitia maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Kibiashara sabasaba, Wadau wa kilimo wameelezea namna wameendelea kuimarisha juhudi za kuongeza tija katika sekta ya kilimo kupitia kuendeleza kilimo ikolojia hai, kuhamasisha matumizi ya mbolea za organic na bidhaa za kibailojia, pamoja na kuwawezesha vijana kushiriki katika kilimo biashara. Mratibu wa Tanzania Organic Agriculture Movement (TOAM), Ernest Jerome, alisema Tanzania tayari ina Mkakati wa Taifa wa Kilimo Ikolojia Hai unaolenga kuboresha upatikanaji wa pembejeo, kuongeza ushirikiano wa wadau na kuwainua wakulima kupitia kilimo endelevu. Wakati huo huo, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, TFRA na Tanzania Fertilizer Company (TFC) inaendelea kushirikiana na wazalishaji wa mbolea za organic na bidhaa za kibailojia ili kuongeza uzalishaji wa pembejeo zinazotengenezwa nchini na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje. Kwa upande wake, Meneja Masoko wa Tanzania Biotech Product Limited (TBPL), Samuel Ponziray, alisema bidhaa za kibailojia zinazozalishwa na kiwanda hicho zimeendelea kusaidia kudhibiti mazalia ya mbu na kuchangia kupungua kwa kiwango cha maambukizi ya malaria nchini kutoka asilimia 14.3 hadi asilimia 5.5, huku Serikali ikilenga kutokomeza malaria ifikapo mwaka 2030. Aidha, Wizara ya Kilimo imewahimiza vijana kutumia fursa za BBT Project One, programu inayotoa mafunzo ya kilimo biashara, mashamba ya pamoja, ufugaji na uwezeshaji wa kifedha ili kuongeza ushiriki wa vijana katika sekta ya kilimo na kuifanya kuwa chanzo cha ajira na ukuaji wa uchumi.