WATUMISHI WAPYA SEKRETARIETI YA AJIRA WATAKIWA KUZINGATIA SHERIA NA KANUNI

Watumishi wapya wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wametakiwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma katika utendaji wao. Wito huo umetolewa na Mhasibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma Christopher Nkupama (CPA) wakati akifungua mafunzo ya awali Kwa watumishi wapya kwa niaba ya Kaimu Katibu wa Ofisi hiyo. "Ndugu washiriki, mkiwa watumishi wa umma mara zote mnapaswa kujua na kuzingatia sheria na kanuni mbalimbali za utumishi wa umma" alisema Nkupama. Aidha, katika ufunguzi huo, Mhasibu Nkupama ameeleza kuwa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma ina matarajio makubwa kwa watumishi hao katika kuhakikisha wanaongeza ufanisi wa kiutendaji. "Tuna matarajio kuwa mtakapofahamu sheria na taratibu mtaongeza ufanisi katika utendaji na uwajibikaji utakuwa mkubwa, kwa kuwa sisi tunawajibika Kwa wananchi na wadau wetu wengine basi mafunzo haya yakatuongezee kitu katika kuwasaidia wananchi" aliongeza. Katika hatua nyingine Mhasibu Mkuu huyo wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira amewapongeza watumishi wapya wa Ofisi hiyo na kuwasisitiza kutekeleza wajibu wao ipasavyo ili kumsaidia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kutimiza malengo ya serikali kwa kutoa huduma bora kwa wananchi. Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Chuo Cha Utumishi wa Umma, Mkurugenzi wa Chuo hicho kutoka ndaki ya Singida Dkt.Hamis Amani ameupongeza uongozi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kwa kuandaa mafunzo hayo kwa watumishi wapya wa ofisi hiyo. "Nawapongeza kwa kuandaa mafunzo haya ambayo yatawafanya washiriki wawe na uelewa wa kina kuhusu utumishi wa umma na kutambua sheria na miongozo ya Utumishi wa umma" alifafanua Dkt.Amani. Vilevile Dkt.Amani amewataka watumishi hao kuzingatia mafunzo hayo ili kutokwamisha utendaji wa serikali na kuchelewesha huduma kwa wananchi. Mafunzo elekezi ya awali kwa watumishi wapya wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma yanafanyika Kwa siku tatu kuanzia Agosti 28 hadi Agosti 30, 2023 jijini Dodoma.