JPM: - “Kama kuna baba zao wanawatuma, watakwenda kuwasimulia vizuri”

Rais John Magufuli amepiga marufuku maandamano yoyote yasiyo halali yenye lengo la kupinga jitihada za serikali na kusema watakaokaidi agizo hilo, vyombo vya dola vimejipanga kukabiliana nao ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria. Rais Magufuli ameyasema hayo leo, wakati wa uzinduzi wa Tawi la Benki ya CRDB huko Chato ambapo pia amewataka Watanzania kuchukia na kuwapuuza watu wanaohamasisha maandamano yasiyokuwa na tija kwa jamii na taifa kwa jumla. Amesema iwapo kuna wanaotaka kuandamana basi wajiandae kujuta ama wasubiri muda wake wa kuwa madarakani uishe. Aidha Rais Magufuli pia amesihi Watanzania kuanza kujifunza kuwa wazalendo wa nchi yao kwa kupinga viashiria vyovyote vya uvunjifu wa amani huku akiwataka viongozi wa dini kutotumia nyumba za Ibada kufanya uchochezi wa kisiasa.