WAZIRI MKUU DKT MWIGULU ALIVYOJIBU HOJA ZA MZINDAKAYA AKIWA ZIARANI RUKWA.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amejibu na kutoa maelekezo mbalimbali kuhusu hoja zilizowasilishwa na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa, Mheshimiwa Jacqueline Mzindakaya, wakati wa ziara yake mkoani humo. Hoja hizo zilihusu sekta mbalimbali za maendeleo ikiwemo miundombinu, afya, biashara na kilimo, ambapo Mheshimiwa Mzindakaya alizipaza sauti kwa lengo la kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazowakabili wananchi wa Mkoa wa Rukwa. Kuhusu suala la miundombinu ya usafiri wa anga, awali Mheshimiwa Mzindakaya alihoji bungeni maendeleo ya ukarabati wa Uwanja wa Ndege wa Sumbawanga. Akijibu hoja hiyo, Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, alieleza kuwa maandalizi ya mwisho yanaendelea na kwamba majaribio ya kurusha ndege yataanza hivi karibuni. Hatua hiyo ilidhihirika Machi 8, 2026 wakati Waziri Mkuu alipotua katika uwanja huo akiwa ziarani mkoani Rukwa. Katika sekta ya afya, Mheshimiwa Mzindakaya aliiomba Serikali kujenga Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Rukwa ili kupunguza adha ya wananchi kusafiri mikoa mbalimbali kutafuta huduma za madaktari na kutumia gharama kubwa za matibabu. Akijibu hoja hiyo, Waziri Mkuu aliagiza mamlaka husika mkoani Rukwa kuwasilisha rasmi ombi hilo Serikalini ili liweze kufanyiwa kazi, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050. Aidha, katika sekta ya biashara, Mbunge huyo aliwasilisha ombi la kufungwa kwa taa katika Soko la Namanyere (Majengo) Wilayani Nkasi, ili kuwawezesha wanawake wajasiriamali wadogo wadogo kufanya biashara zao hadi nyakati za usiku kwa usalama zaidi. Katika sekta ya kilimo, Mheshimiwa Mzindakaya alihoji utekelezaji wa mradi wa skimu ya umwagiliaji katika Kijiji cha Katongolo. Akijibu hoja hiyo, Naibu Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa David Silinde, alieleza kuwa serikali inaendelea kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unakamilika na kuwanufaisha wananchi. Akihitimisha, Mheshimiwa Jacqueline Mzindakaya alimshukuru Waziri Mkuu kwa namna anavyosikiliza na kujibu hoja za wananchi. #gachitvonlineupdates #gachitv #gachitvonline