Moravian Choir - Wale Wayunani.

Wimbo huu wa Wale Wayunani umeimbwa na Kwaya ya Moravian kutoka Mbalizi jijini Mbeya. Wimbo unahusu watu waliotaka kumuona Yesu ambao walikuwa Wayunani (Wagiriki) walioenda kuabudu wakati wa sikukuu ya Pasaka huko Yerusalemu. Tukio hili linapatikana katika Injili kama alivyoiandika Yohana Mtakatifu 12:20–22. Neno la Mungu linasema: "Palikuwa na Wayunani kadha wa kadha miongoni mwa watu waliokwea kwenda kuabudu kwenye sikukuu. Basi hao walimwendea Filipo, mtu wa Bethsaida ya Galilaya, wakamwomba, wakisema, Bwana, sisi tunataka kumwona Yesu. Filipo akaenda, akamwambia Andrea; kisha Andrea na Filipo wakamwambia Yesu." Kwa nini walimwendea Filipo? • Filipo alikuwa na jina la Kigiriki, hivyo iilikuwa rahisi kwa Wayunani kuwasiliana naye. • Pia, Filipo alikuwa anatoka Bethsaida ya Galilaya, eneo lililokuwa na mchanganyiko wa Wayahudi na watu wa mataifa mengine. Tukio hili linaonyesha kwamba huduma ya Yesu haikuwahusu Wayahudi pekee, bali pia mataifa mengine. Hivyo, wokovu ni kwa watu wote. Wayunani walikuwa watu wa mataifa (si Wayahudi). Kuja kwao kumtafuta Yesu kulionyesha kwamba, muda ulikuwa umefika ambapo ujumbe wa Yesu unaenea kwa ulimwengu mzima, si kwa Israeli tu. Jambo hili limeelezwa kama agizo la kuhubiri injili kwa mataifa yote (Mathayo 28:19 - 20). Neno la Mungu linasema: "Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari."