BENKI YA TIB NA KAMPUNI YA TIB RASLIMALI LTD WAAINISHA FURSA NA KUELIMISHA WANANCHI KUPITIA SABASABA
Benki ya Maendeleo ya TIB pamoja na TIB Rasilimali Limited zimetumia Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma za mikopo ya maendeleo na fursa za uwekezaji katika soko la mitaji. Akizungumza katika maonesho hayo, Afisa wa Benki ya Maendeleo ya TIB, Eugene Naphtal Ingwe, alisema benki hiyo ya serikali imeendelea kufadhili miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, viwanda, huduma, maji, nishati, madini na miundombinu, sambamba na kuwawezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati (SMEs). Alisema ushiriki wa TIB katika maonesho hayo unalenga kuwaelimisha wawekezaji na wajasiriamali kuhusu namna wanavyoweza kunufaika na mikopo ya maendeleo ili kukuza biashara na miradi yao. Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Kukuza Biashara na Alternative Channels wa TIB Rasilimali Limited, Lamek Mwavipia, alisema kampuni hiyo inatoa ushauri wa uwekezaji kwa watu binafsi, kampuni na taasisi zinazotaka kuwekeza katika hisa na hati fungani. Alisema TIB Rasilimali Limited pia inatoa ushauri bila malipo, husaidia kufungua akaunti za CDS na kuwaelekeza wananchi kuhusu fursa zilizopo katika soko la mitaji, huku akiwakaribisha kutembelea banda la Wizara ya Fedha na Mipango ili kupata elimu zaidi kuhusu huduma zinazotolewa na taasisi hizo mbili.
