Sheikh Othman Maalim - Misingi ya kuchagua mke anayefaa kuoa

Sheikh Othman Maalim - Misingi ya kuchagua mke anayefaa kuoa Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu sifa zinazohitajika katika kuchagua mke. Uislamu ikiwa ndiyo Dini ya kimaumbile imetupatia muongozo katika kila nyanja ya maisha pamoja na kuchagua mke, ambaye ni mshirika wa mwanaume wa maisha. Miongoni mwa sifa zinazohitajika katika kuchagua mke ni: 1. Mwanamke kuwa na Dini, tabia na maadili mema. Ama mas-ala ya Dini ni ile Hadiyth ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘Alayhi wa aalihi wa sallam) aliyosema: Chagua mwenye Dini usije ukapata hasara (al-Bukhaariy na Muslim). Dini si ya kinadharia bali imfanye abadilike katika mambo yake yote kama kuwa na tabia njema na maadili mema. 2. Kumpendeza mume anapomuangalia. Kupendeza na uzuri ni vitu ambavyo kila mwanamme ana kile anachokiona kuwa ni kizuri. Ndiyo nasaha aliyotoa Mtume (Swalla Allaahu ‘Alayhi wa aalihi wa sallam) kwa Mughiyrah bin Shu‘bah (Radhiya Allaahu ‘anhu): Kamwangalie kwali kufanya hivyo kutaleta mapenzi baina yenu (an-Nasaa’iy). 3. ni mwenye kuingiliana na watu na mwenye moyo wa bashasha kabisa. Mafungano ni baina ya familia mbili, yako na yake. Kwa ajili hiyo anatakiwa awe ni mwanamke mwenye kufanya mahusiano na watu wako wa karibu ili kuwe na maendeleo na uhusiano mwema. 4. Mwenye kuzaa, na hili kama wanavyuoni walivyosema ni kuangalia kizazi cha madada zake na jamaa zake wa karibu Hata hivyo, muhimu zaidi ni Dini na ikiwa ana sifa nyingine ziwe ni baada ya hiyo sifa ya kwanza. Ama kuhusu sifa njema na nzuri ambazo kwayo mwanamme anafaa achague mkewe na mwanamke naye achague mumewe ni kama zifuatazo kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu: KUCHAGUA KWA MSINGI WA DINI: Huu ni msingi wa kwanza na muhimu sana. Ukweli ni kuwa kila mmoja ana sifa ambayo anaona lau atapata mwendani wake basi ashafika kwenye kilele katika maisha yake. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) naye ametuelezea pale aliposema: “Mwanamke huolewa kwa sababu NNE: Kwa mali yake, nasaba yake, uzuri wake na Dini yake, Tafuta mwenye dini uwe salama (yaani usiharibikiwe katika maisha yako)” (al-Bukhaariy na Muslim). Amesema tena: “Akikujieni ambaye mumeridhika na dini na maadili yake, muozesheni. Msipofanya hivyo kutakuwa na fitna katika ardhi na ufisadi mkubwa” (at-Tirmidhiy). Amesema tena (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam): “Mwenye kumuoa mwanamke kwa sababu ya mali yake Allah hamzidishii ila ufukara; mwenye kumuoa kwa sababu ya nasaba yake, Allah Atamtweza; mwenye kuoa kwa ajili ya kuinamisha macho yake, kulinda uchi wake au kuunganisha kizazi, Allah atambarikia kwayo na atabarikiwa kwake” (atw-Twabraaniy). #SheikhOthmanMaalimMisingiyakuchaguamkeanayefaakuoa #SheikhOthmanMaalimmkeanayefaakuoa #OthmanMaalimmkeanayefaakuoa #Misingiyakuchaguamkeanayefaakuoa #mkeanayefaakuoa #mwanamkeanayefaakuoa #sifazakuchaguamke KUFADHILISHA MWANAMKE MWENYE KUZAA: Alikuja mtu kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamuuliza: “Ewe Mtume wa Allah mimi nampenda mwanamke mwenye nasaba nzuri, cheo na mali isipokuwa hazai, je nimuoe?” Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamkataza. Akarudi tena mara ya pili na ya tatu akajibiwa: “Oeni wanawake wenye mapenzi na wazazi, ili nipate kujifakhiri kwa Umma zingine siku ya Qiyaamah” (Abu Daawuud, an-Nasaa’iy na al-Haakim). Waallahu Aalam Barakallaahu feeykum