Viongozi vyama vya ushirika wahimizwa kuzingatia weledi.
Viongozi vyama vya ushirika wahimizwa kuzingatia weledi. Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Mhe. Dustan Kyobya, amewataka Viongozi wa Vyama vya Ushirika Mkoani Morogoro kuzingatia weledi wa kazi zao ikiwemo kuwa waaminifu, kuwa wa wazi, ushirikishwaji, kuiishi miiko ya uongozi na haki na kuwa wabunifu ili kuongeza ufanisi pamoja na kuondoa migogoro ndani ya vyama hivyo. Kyobya ametoa Wito huo Juni 24, 2026 wakati wa Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Morogoro lililokuwa na kaulimbiu inayosema “Ushirika kwa Dunia Yenye Amani”. Jukwaa hilo lililofanyika mji mdogo wa Ifakara Wilayani Kilombero limehusisha viongozi mbalimbali wa vyama vya ushirika kutoka mkoa huo. Akizungumza katika jukwaa hilo, Mhe. Kyobya amesema kuwa ili kuhakikisha vyama vya ushirika vinaendeshwa kwa weledi, ni muhimu viongozi wake wakapewa elimu na mafunzo ya mara kwa mara ili kuongeza ufanisi wa utendaji wao. “Nitoe msisitizo kwa watumishi wa vyama vya ushirika kuzingatia weledi, uaminifu, uwazi, ushirikishwaji, miiko ya uongozi, ubunifu na haki,” amesisitiza Mhe. Dustan Kyobya. Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amewataka viongozi hao kuepuka vitendo vya rushwa, akieleza kuwa vitendo hivyo husababisha migogoro ndani ya vyama vya ushirika na kuharibu taswira ya sekta hiyo. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utafiti na Mafunzo wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Grace Masambaji, amesema vyama vya ushirika vinapaswa kujikita zaidi katika shughuli za kibiashara ili kuongeza tija kwa wanachama wake, na kuonesha umuhimu wa kujenga miundombinu ya kuhifadhi mazao, kutumia mizani ya kidijitali katika upimaji wa mazao hayo. Naye Msajili Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Morogoro, Bi. Cesilia Sosteness, amesema katika msimu wa 2026/27 vyama vyote vya ushirika mkoani Morogoro vitatumia mizani ya kidijitali kupima mazao, hatua ambayo amesema itasaidia kujenga uwazi na kuongeza imani kwa wakulima. Katika hatua nyingine amesema Kamati ya Elimu imefanikiwa kuendesha mafunzo kwa watendaji 489 katika mwaka wa fedha 2025/26 kuhusu mbinu bora za uendeshaji wa vitabu vya hesabu na ufungaji wa hesabu za vyama vya ushirika. Mwenyekiti wa Jukwaa hilo akisoma risala kwa niaba ya wanaushirika ameiomba Serikali na taasisi husika kuzingatia maombi mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kufanya mapitio ya baadhi ya tozo na kodi zinazowakabili wakulima, kusimamia matumizi bora ya ardhi katika vijiji, kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wafugaji wanaoingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima, pamoja na kutafuta masoko. Mwisho.
