TANZANIA NA BURUNDI KUANZA UJENZI WA RELI YA KISASA / TANZANIA NA BURUNDI KUANZA UJENZI WA SGR.

TANZANIA NA BURUNDI KUANZA UJENZI WA SGR. Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa na Rais wa Burundi Meja Jenerali Evariste Ndayishimiyiye, wameweka jiwe la msingi la ujenzi wa reli ya kisasa SGR ya kutoka Uvinza Kigoma Tanzania hadi Musongati nchini Burundi yenye urefu wa kilomita 240, ikiwa ni reli ya kwanza itakayounganisha nchi na nchi katika ukanda wa Afrika Mashariki. Akizungumza katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi uliofanyika eneo la Musongati, katika mkoa wa Buruga nchini Burundi, Waziri Mkuu ambaye amemwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan, amesema utekelezaji wa mradi huo ni matunda ya ushirikiano baina ya nchi hizo ulioanzishwa mwaka 1975. Amesema kuwa mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya nchi hizo na ajenda ya umoja wa Afrika ya mwaka 2063. Ameongeza kwamba mradi huo unalenga kuimarisha na kupanua miundombinu ya usafirishaji kati ya nchi hizo ili kurahisisha, kupunguza gharama na kuongeza ufanis wa shughuli za kibiashara na uhusiano uliopo wa wa kijamii baina ya nchi hizo na maeneo mengine ya ukanda wa Afrika wa Mashariki. Kwa upande wake, Rais wa Burundi, Meja Jenerali Evariste Ndayishimiye, amesema kuanza kwa ujenzi wa reli hiyo kutatibu shauku ya muda mrefu ya nchi hiyo kuwa na usafiri wa reli. Awali Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, amesema kukamilika kwa ujenzi wa reli hiyo itaboresha maisha na uchumi wa wananchi wa pande zote mbili kwa kupunguza gharama za usafirishaji wa bidhaa kati ya Tanzania na Burundi. Hatua ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa reli ya kisasa SGR kutoka Uvinza hadi Msongati, imewafurahisha wananchi wa pande zote mbili ambao wamesema itawaletea maendeleo.