BRELA YAJA NA MUAROBAINI WA MIGOGORO KATIKA KAMPUNI

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) inakutana na wadau wenye migogoro katika kampuni mbalimbali ili kuwezesha kampuni hizo kufanya kazi kama ilivyokusudiwa katika uanzishwaji wake. Akizingumza katika siku ya kwanza ya wiki maalum ya "Suluhisha na BRELA" inayofanyika katika Ukumbi wa Makumbusho ya Taifa, uliopo Mtaa wa Shaaban Robert, Jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Makampuni na Majina ya Biashara kutoka BRELA, Bw. Meinrad Rweyemamu amesema, kampuni zinaweza kuendeshwa bila migogoro endapo uendeshwaji wake utazingatia Sheria. Rweyemamu amewataka wamiliki wote wa kampuni ambao wanakumbana na changamoto katika uendeshaji wa kampuni zao, kufika na kupatiwa huduma, kwani Msajili ametoa muda wa wiki moja ambapo migogoro katika kampuni itapatiwa ufumbuzi kwa kushauriana na wataalamu kutoka BRELA.