MSHINDI WA KWANZA WA WAZO BUNIFU 2025 AELEZEA SAFARI YA USHINDI, ATOA HAMASA KWA WABUNIFU

Mshindi wa kwanza wa shindano la Wazo Bunifu 2025, Bw. Gabriel Mashenene, aliyefanikiwa kujinyakulia zawadi ya Shilingi milioni 50, ameelezea safari yake ya ushindi huku akitoa hamasa kwa vijana wa Tanzania na wabunifu wote kujitokeza kwa wingi kushiriki mashindano hayo bila kusita. Amesisitiza kuwa ubunifu unahitaji uthubutu na kujiamini, akiwataka wabunifu kutumia fursa zilizopo kuwasilisha mawazo yao yenye tija kwa maendeleo ya taifa. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeendelea kuwahamasisha wananchi kushiriki katika mashindano ya Wazo Bunifu yanayolenga kupata suluhisho za kibunifu zitakazochangia kuboresha mfumo wa kodi nchini, ambapo washiriki wanapata fursa ya kushindania zawadi ya hadi Shilingi milioni 50. Mawazo yanayowasilishwa yanapaswa kulenga kupanua wigo wa kodi, kurahisisha ukadiriaji na ulipaji wa kodi kwa biashara ndogo ndogo, kuimarisha huduma za kidijitali, kupunguza gharama za ukusanyaji wa mapato, pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa kama AI, Big Data na Blockchain, huku yakiboresha pia utatuzi wa migogoro ya kodi. Mwisho wa kutuma mawazo ni Julai 31, 2026.