Mwenyekiti Gabriel Mwakagenda Apongeza Serikali Baada ya Lupoto Kunufaika na Mradi wa Milioni 196

*MWENYEKITI WA HALMASHAURI YA WILAYA YA RUNGWE APOKEA VIFAA VYA KUFUNDISHIA KILIMO SHULE YA SEKONDARI LUPOTO Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Ibighi, Gabriel Mwakagenda, amepokea vifaa vya kufundishia na kujifunzia somo la kilimo katika Shule ya Sekondari Lupoto iliyopo Kata ya Ibighi, Wilaya ya Rungwe. Akizungumza wakati wa makabidhiano ya vifaa hivyo, Mwenyekiti Mwakagenda ameishukuru Serikali kwa kuichagua Shule ya Sekondari Lupoto kunufaika na mradi huo, ambapo zaidi ya shilingi milioni 196 zimetolewa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kufundishia somo la kilimo. Amesema uwekezaji huo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuboresha mazingira ya elimu kwa vitendo na kuwawezesha wanafunzi kupata maarifa yatakayowasaidia kujitegemea na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini. Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Lupoto amesema vifaa hivyo vitasaidia kuongeza ufanisi wa ufundishaji na ujifunzaji wa somo la kilimo, huku vikitoa nafasi kwa wanafunzi kujifunza kwa vitendo na kuongeza kiwango cha ufaulu. Ameongeza kuwa maarifa na ujuzi watakaoupata wanafunzi kupitia vifaa hivyo utawasaidia wanapohitimu masomo yao na kurejea katika jamii, ambapo wataweza kutumia elimu hiyo kujiajiri na kuongeza uzalishaji katika sekta ya kilimo.