ST.GASPAR REFERRAL AND TEACHING HOSPITAL ITIGI YAZINDUA KITENGO CHA MATIBABU YA WATOTO WACHANGA-NICU

Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa na Mafunzo St.Gaspar Itigi Fr.Justin Boniface C.P.P.S amesema kukamilika kwa Kitengo cha NICU kutasaidia kuokoa uhai wa watoto wengi wachanga wenye changamoto mbalimbali za kiafya. Fr.Justin Boniface C.P.P.S amebainisha hayo katika hotuba yake iliyo somwa na Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa na Mafunzo St.Gaspar Itigi Dkt.Simon Mrema katika uzinduzi wa Wodi/kitengo cha matibabu kwa watoto wachanga wenye umri kuanzia siku 0-28 itakayotoa huduma za kawaida ,huduma kwa watoto njiti(premature babies)na huduma za uangalizi maalumu kwa watoto wachanga.(NICU) Katika hutuba yake Mkurugenzi amesema kuwa kukamilika kwa Kitengo hicho ni alama ya uponyaji,huruma na ushuhuda wa yale tunaweza kufanikisha tunaposhirikiana pamoja katika kuwatumikia wanadamu “Huu si mradi tu bali ni uwekezaji muhimu kwa mustakabali wa taifa letu,familia zetu na dunia kwa ujumla”amesisitiza Fr.Justin Boniface C.P.P.S Aidha Mkurugenzi amewashukuru washirika wa taasisi yetu Dental Legacy Foundation kwa ukarimu wao, maono na Imani yao katika utume wetu ndio vimetufikisha hapa na kwamba ujenzi umekamilika na kilichobaki ni usimikaji wa vifaa muhimu vya kitabibu ili Kitengo kianze kufanya kazi kikamilifu “Tumekubaliana pamoja na taasisi ya Dental Legacy Foundation kuendelea kukiwezesha kitengo hiki kuwa cha kisasa,kinachofanya kazi kikamilifu ili kiweze kuokoa uhai wa watoto wengi wachanga”amesema Fr.Justin Boniface C.P.P.S Pia Mkurugenzi ametumia fursa hii kupongeza timu nzima ya Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya St. Gaspar kwa kujitolea bila kuchoka,kwa huruma na sadaka kila siku na kwamba huo ndio msingi wa kila mafanikio tunayosherehekea leo.